`

Home » » WAZAZI WILAYANI NANYUMBU WAONESHA KUTORIDHISHWA NA ELIMU KUNAKOSABABISHA KUFELI KWA WATOTO WAO.

WAZAZI WILAYANI NANYUMBU WAONESHA KUTORIDHISHWA NA ELIMU KUNAKOSABABISHA KUFELI KWA WATOTO WAO.

Na mwandishi wetu.

Nanyumbu. 

WAZAZI wilayani Nanyumbu mkoani Mtwara imeelezwa kuchoshwa mechoshwa na hali ya elimu wilayani humo kutokana na kushika nafasi ya mwisho kila mwaka na kuamua kuanzisha mikutano na wazazi kila kata kutoa hamasa na kuwaelimisha ili kuinua kiwango cha elimu ambacho kwa sasa ni janga kubwa ndani ya wilaya hiyo.

Akizungumza na wazazi, viongozi na walimu katika mkutano huo, Mkuu wa wilaya hiyo Festo Kiswaga alisema kuwa ili wilaya hiyo isonge mbele na kushika nafasi za juu kimkoa na kitaifa lazima wazazi, viongozi na walimu washirikiane na kutimiza wajibu wao.

"Kwa siku ya leo napenda tushirikiane changamoto inayohusu moja kwa moja jamii kuwa na mtazamo hasi juu ya elimu na kutoipatia kipaumbele, hii ni changamoto kubwa na ambayo ndio msingi wa changamoto nyingine,"alisema Kiswaga.

Alisema kuwa ndani ya changamoto hiyo kuna mambo mengine ambayo ni pamoja na wazazi kutohimiza watoto wao kuhudhuria shuleni ipasavyo, kutohudhuria vikao vya shule ili kujadili masuala yahusuyo shule.

Aliongeza kuwa wazazi pia kuwaamuru watoto wasifanye vizuri katika mitihani ya darasa la saba ili wasichaguliwe kuendelea na masomo ya sekondari ili wasibugudhiwe tena na serikali kuwataka kuwasomesha.

"Mambo haya ni madogo yanapotamkwa lakini shughuli za maendeleo ni kubwa kwa kuwa athari zake ni mbaya na za muda mrefu kusanyiko hili ni kujaribu kufufua hamasa ya wananchi katika kushiriki kwenye shughuli za elimu kwa hali na mali,"alisema.

Naye Afisa Elimu wa Wilaya hiyo, Angelina Makwaya alisema kuwa mikutano hiyo itafanywa kila kata ili kuwapatia elimu wazazi ili wajue umuhimu wa elimu kwa watoto wao ili kujenga taifa la wasomi.

"Kikubwa sisi kama wenye dhamana ya kusimamia elimu tumechoshwa na kuwa wa mwisho kielimu kimkoa na kitaifa hiyo hamasa hii itatufanya tuamshe elimu na kufanya vizuri kila kwa ngazi zote,"alisema Makwaya.

Alisema kuwa wazazi wa wilaya hiyo hawana muamko wa elimu ambapo wanaona ni kawaida kwa mtoto kwenda disko na video usiku bila kujua shuleni amefanya nini  na maendeleo yake yapoje kitu kinachokwamisha sekta ya elimu.

Mmoja wa wazazi waliohudhuria mkutano huo, Augustino Mapunda alisema kuwa suala la wazazi kutojua umuhimu wa elimu kwa watoto wao ni changamoto ambayo inazidisha vijana wengi wasiojua kusoma na kuandika.

"Ukizunguka ndani ya wilaya hii utakutana na vijana wengi vijiweni wakicheza Pool table  na madereva pikipiki hawajui kusoma wala kuandika sijui wazazi wenzangu wanafikiria nini kwa watoto wao hili ni janga kubwa kwa wilaya yetu,"alisema Mapunda.

Wilaya ya Nanyumbu tangu imeanzishwa mwaka 2006 ikitokea wilaya ya Masasi bado inafanya vibaya katika elimu ya msingi na sekondari hali inayotishishia ustawi wa elimu wilayani humo na kuendelea kuzalisha vijana wasiokuwa na ajira ambao wanabaki kukaa vijiweni na kuilaumu serikali baada ya kuwalaumu wazazi wao.

MWISHO……………..

0 comments:

Post a Comment

 
Designed By | Wishes co |
Copyright © 2014. Jicho La Mdadisi - All Rights Reserved
Template Modify by
Proudly powered by Wishes INK